Home » » WAZIRI MKUU AWATEGA WAPINZANI

WAZIRI MKUU AWATEGA WAPINZANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
Waziri  Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema tamko la katazo la mikutano ya kisiasa nchini, lilitafsiriwa vibaya kwa kuwa alizungumzia hali ya jimbo lake alipokwenda kuwashukuru wananchi, ingawa alikataa kulifuta na kuvitaka vyama kufuata sheria.
 
Kauli ya Majaliwa ilitokana na swali aliloulizwa na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu.
 
Katika swali lake, Mbowe alisema kauli hiyo ya Waziri Mkuu, aliyoitoa akiwa jimboni kwake Ruangwa, inalenga kufifisha demokrasia na kuzuia vyama vya siasa kutimiza majukumu yao. 
 
Akijibu swali hilo, Majaliwa alisema uongozi wa serikali ya awamu ya tano unafuata misingi ya kidemokrasia, sheria, kanuni na katiba.
“Suala la katazo kwa vyama vya siasa kufanya mikutano, msemaji wa kwanza hakufanya kazi yake vizuri. Hii kauli niliitolea jimboni kwangu nikiwa  Mbunge na nilikuwa sijavaa koti la uwaziri mkuu.
 
“Nilikutana na makundi mengi, polisi, watumishi wa halmashauri na madiwani wakiwamo wa vyama vya upinzani, ambaao walisema sasa tufanye kazi na siasa pembeni na mimi nikasema ni kweli walioshinda ndio wafanye kazi wakutane na wananchi,” alisema.
 
Aliongeza kuwa: “Kauli yangu ilitokana na mazingira yale, lakini likichukuliwa na maeneo mengine si vibaya, kwa hiyo kama mwandishi aliyeandika ile habari ya kwanza angeendelea kufuatilia niliyoyasema kwenye ziara yangu yote ile jimboni, mkanganyiko huu usingekuwapo,” alisema Majaliwa.
 
Baada ya jibu hilo, Mbowe alimtaka Majaliwa kubatilisha kauli yake ya awali kwa maelezo kwamba yeye ni kiongozi kwa hiyo chochote anachozungumza kinachukuliwa kama amri halali.
 
Hata hivyo, Majaliwa hakuikanusha kauli yake ya awali licha ya kusema nchi inaongozwa na Katiba, kuna sheria zinazoiongoza hivyo kama chama cha siasa kinataka kufanya mikutano, kifuate sheria.
 
Pia Mbowe alitaka Majaliwa afafanue kauli ya serikali juu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kutorusha moja kwa moja majadiliano bungeni.
 
Kuhusu swali hilo, Majaliwa alisema TBC ilichofanya ni kubadilisha ratiba ambapo sasa itakuwa ikirusha kipindi cha maswali na majibu asubuhi na kisha majadiliano kurekodiwa na kuonyeshwa usiku.
 
Kwa upande wake, Mbunge wa Babati Mjini (Chadema), Pauline Gekul, alimwuliza Waziri Mkuu juu ya mkanganyiko wa elimu bure ambapo wanafunzi wa bweni wanalipiwa fedha ya chakula shuleni lakini wale wa kutwa waambiwa walipie chakula.
 
Majaliwa alikiri kuwapo kwa mkanganyiko kwenye suala la elimu bure na kuwa hivi karibuni serikali itatoa mwongozo unaojitosheleza juu ya utekelezaji wake.
 
Alisema baadhi ya mambo ambayo serikali itagharimia kwenye elimu bure ni Sh. 20,000 ya ada kwa shule za sekondari za kutwa, Sh. 70,000 za ada kwa shule za bweni, fedha za mitihani za darasa la nne na kidato cha pili pamoja na gharama za chakula kwa shule za bweni.
 
Naye Mbunge wa Ilala (CCM), Mussa Zungu, alitaka serikali itofautishe viwango vya kodi ya ongezeko la thamani (VAT), kufuatana na ukubwa wa biashara, jambo ambalo litasaidia kuwafanya walio wengi kulipa kodi hiyo na kuinua pato la taifa.
 
Alisema moja za nchi jirani, ambayo hakuitaja, ilipunguza VAT kwa biashara zisizo rasmi mwaka 2009 na ikafanikiwa kukusanya Sh. trilioni nane. 
 
Akijibu swali hilo, Majaliwa alisema ombi kama hilo amewahi kulipata tena alipokutana na wafanyabishara, lakini linahitaji utafiti wa kina kwa sababu linaweza kuleta usumbufu wakati wa utekelezaji wake.
 
Alisema wasiwasi mkubwa uko kwenye tathmini ambapo ni rahisi maofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kuingia kwenye mitego ya rushwa na kuwasumbua wananchi.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa