Home » » MJAMZITO AJIFUNGULIA SAKAFUNI

MJAMZITO AJIFUNGULIA SAKAFUNI

na Danson Kaijage, Dodoma
MAMA mjamzito, Sarah Malima (17), mkazi wa Michese, amenusurika kufa na baada ya kujifungulia chini ya sakafu wodini katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma kutokana na manesi kushindwa kumhudumia huku wakimtupia maneno ya kejeli.
Tukio hilo lilitokea hospitalini hapo jana baada ya mama huyo kuwataka manesi waliokuwapo kumsaidia baada ya kuzidiwa na uchungu.
Sarah alisema kabla ya kujifungulia wodini, aliwaomba manesi kumpeleka chumba cha kujifungulia, lakini hawakumsikiliza na badala yake waliendelea kula chips huku wakimtolea maneno ya kebehi.
Tanzania Daima ilishuhudia tukio hilo ambalo liliwasikitisha watu waliokuwa hospitali hapo na mama huyo alisema kuanzia saa 10:30 jioni aliwaambia manesi wamsaidie, lakini hawakumsikiliza.
“Nilianza kuwaelezea muda mrefu manesi wanisaidie, kwani nilikuwa nasikia uchungu, lakini nilikuwa nikijibiwa majibu ya ovyo na baadaye waliniambia nisiwashobokee kwani wanakula.
“Niliendelea kujisikia vibaya hadi kufikia hatua ya kujifungulia sakafuni, jambo ambalo ni hatari, lakini namshukuru Mungu kwani nimenusurika kufa kutokana na uzembe wa manesi hawa,” alisema.
Kwa upande wao manesi waliohusika na tukio hilo hawakutaka kuzungumza jambo lolote walipoulizwa kwa madai kuwa wao si wasemaji.
Naye Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Nassoro Mzee, alipoulizwa alisema kuwa hilo ni tatizo dogo inashangaza kuona watu wanalilalamikia.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa