Home » » ‘Mliofungiwa viwanja ombeni Jamhuri Dom’

‘Mliofungiwa viwanja ombeni Jamhuri Dom’

MENEJA Msaidizi wa Uwanja wa Jamhuri Dodoma , Saidi  Kalela, amezishawishi timu za Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi Daraja la Kwanza ambazo viwanja vyake vimefungiwa na havifai kutumika kwa mashindano, viombe kutumia huo.
Viwanja vilivyofungiwa ni Ali Hassan Mwinyi Tabora, Mkwakwani Tanga, Kaitaba Bukoba, Jamhuri Morogoro, Sokoine Mbeya, Majimaji Songea na Sheikh Amri Abeid Arusha.
Kalela alijipigia upatu huo, baada ya kuhojiwa na Tanzania Daima wanafanya jitihada gani ili uwanja huo usikumbwe na panga la Bodi ya Ligi nchini (TPL-Board), lililovipitia viwanja saba kutokana na kutokuwa na hali nzuri.
Akijibu, Kalela alijinasibu kuwa anazishawishi timu za Ligi Kuu na Daraja la Kwanza ambazo viwanja vyake vimefungiwa, ziombe kuutumia Uwanja wa Jamhuri Dodoma kwa sababu una hali nzuri, sambamba na hamasa ya wadau kushuhudia mapambano ya soka.
“Mbali ya uzuri wa Uwanja wa Jamhuri, hapa ni katikati ya nchi, pana mapato ya kutosha, miundombinu inayostahili, unafuu wa maisha na uwezekano wa kusafiri kokote na kwenda popote katika pembe ya Tanzania,” alisema Kalela.
Kalela aliongeza kuwa ushirikiano wao mzuri na Katibu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mkoa, Albert Mgumba, wanaomiliki uwanja huo, ndio unaofanya usiwe katika hali mbaya.
“Tumetoa mwanya kwa wadau wetu, kama ninyi waandishi, mashabiki wa michezo yote, marefa, wachezaji, viongozi wa vyama na serikali, wananchi, wageni wanaotutembelea kimichezo na wabunge wakiwa bungeni, kutukosoa na kutuelekeza palipo pabaya ili turekebishe na kupaboresha,” alisema na kuongeza: “Kimsingi tunakubali changamoto, tukiambiwa pale panasababisha dimbwi la maji, vyoo au milango ina shida, uchafu na mahali popote panapohitaji matengenezo, tunakubali kupafanyia kazi kwa ushirikiano, bila kumrushia huyu koleo la mchanga kuwa ndiye anayehusika.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa