WAKAZI wa eneo la Kisasa ‘C’ Center katika Halmashauri ya Dodoma
wametangaza mgogoro wa viwanja kati ya Mamlaka ya Ustawishaji Makao
Makuu (CDA) na kamati ya kijiji ya kushughulikia upimwaji viwanja.
Wakazi hao wamemuomba Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
Profesa Anna Tibaijuka kuushughulikia haraka ili kuepusha madhara
yanayoweza kutokea.
Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti katika
mkutano waliouitisha kupinga maeneo yao kupewa watu wengine, walisema
wanaweka azimio la kuhakikisha hakuna mtu atakayeingia katika eneo hilo
kujenga kama wenyeji hawajapatiwa viwanja.
“Eneo hili tangu mababu na mababu tulikuwa tunalima na tunaishi hapa,
lakini miaka ya hivi karibuni CDA walikuja na kutueleza wanataka
kupima viwanja, ili mji uweze kujengeka katika mpangilio.
“Sisi hatukukataa. Tulitaka kulipwa na kupewa viwanja kwa ajili ya
kujenga na kwa kuwa tuna watoto na wajukuu na maeneo haya ni yetu kwa
miaka mingi, tulikubaliana kila mtoto ambaye amejenga banda apewe
kiwanja jambo ambalo mpaka sasa halijafanyika,” alisema mmoja wa wakazi
hao.
Walisema waliteua kamati ya kufuatilia upimaji wa viwanja, lakini cha
kushangaza hawajapewa viwanja badala yake wamepewa wageni.
Balozi wa mtaa huo, Wiston Kyeju, alisema kitendo cha wakazi wa
maeneo ambayo yalipimwa viwanja kukosa na kupatiwa watu wengine
kinaweza kusababisha uvunjifu wa amani.
Grest Wiston aliituhumu kamati ya kijiji ya kusimamia viwanja kwa
madai wamefanya kinyume na matarajio ya wananchi ambao waliamini
watawasaidia kuwatetea kupata viwanja.
Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment