Home » » CHADEMA "WAMVAA" KINANA

CHADEMA "WAMVAA" KINANA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimesema propaganda za Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Abdulrahman Kinana juu ya mjadala wa Katiba Mpya unaoendelea bungeni mjini Dodoma, una dhamira ya kuvuruga mwelekeo wa Bunge hilo na kwenye hatua ya kamati.
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa chama hicho, Bw. John Mnyika, aliyasema hayo jana mjini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya kile alichokisema Bw. Kinana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika juzi Dar es Salaam.
Alisema Rais Jakaya Kikwete alipolihutubia Bunge hilo, aliharibu mwelekeo wa mjadala huo kwa kuzungumzia mambo yaliyohusu masilahi ya CCM lakini hali ikapoa baada ya wadau mbalimbali kujadili hotuba hiyo na kutofautiana na Rais kwenye mambo yanayohusu mchakato mzima wa katiba.
“CCM imeamua kufanya propaganda nje ya Bunge hili kwa kuitisha mkutano wenye lengo la kumpongeza Rais Kikwete kwa hotuba yake jambo ambalo ni sawa na kuurudisha tena mjadala kuhusu msimamo wa Rais bungeni.
“Ifahamike kuwa, ule haukuwa msimamo binafsi wa Rais bali wa CCM na ushahidi upo katika waraka wao wa siri uliowasilishwa kwenye Kikao cha Halmashauri Kuu,” alisema Bw. Mnyika.
Aliongeza kuwa, katika waraka huo CCM imesema muundo wa Muungano ndio moyo wa rasimu na ndio unaoamua ibara nyingine ambapo chama hicho kinafahamu ukubwa wa muundo kwenye mjadala wa Katiba, lakini bado wanawadangaya wananchi.
“Maoni ya Watanzania yanataka kubadilishwa ili yaendane na sera ya CCM...sisi tutaendelea kusimamia msimamo na maoni ya wananchi, mkutano wa Kinana aliofanya juzi, umeonesha wazi kuwa chama chake kimeanza kuiponda Tume ya Mabadiliko ya Katiba,” alisema.
Bw. Mnyika alisema tume hiyo ilikusanya maoni ya muundo wa Serikali tatu hivyo CCM imeishiwa hoja kwa kuona kuwa Rasimu ya Pili ya Katiba imezingatia msimamo walioutoa wananchi si vinginevyo.
Aliwataka Watanzania kufahamu kuwa, rasimu hiyo ni matokeo ya uchambuzi wa wataalamu na wananchi wenyewe hivyo CHADEMA haitakuwa tayari kukwamisha mchakato huo ikitambua kuwa tume hiyo haikuwa ya mtu mmoja na maoni waliyotoa yapo sahihi.
Aliwahadharisha wajumbe wa Bunge hilo kutoka CCM, kuhakikisha hawaligeuzi kuwa sehemu ya kuwajadili waliotoa hoja zao juu ya Rasimu ya Katiba na kutopeleka katika kamati zao agenda iliyosemwa na Kinana.
“CCM isiseme maoni ya Jaji mstaafu Joseph Warioba yawekwe pembeni kwa kuwa hayakuzingatia maoni ya mabaraza huku ni kuvuruga mjadala mzima wa katiba,” alisema.
Bw. Mnyika alisema, katika mkutano huo Bw. Kinana alidai haoni umuhimu wa Katiba Mpya kwani Katiba ya zamani watu wengi hawaijui na kusisitiza hata ikiandikwa itaishia kabatini jambo ambalo ni baya kusemwa na kiongozi wa CCM.
Alisema kauli hiyo ni ishara tosha kuwa kuna tatizo kubwa nchini ambalo linashuhudiwa na waraka wa chama hicho ambao unakiri kuwa kuna tatizo la kuvunjwa kwa matakwa ya katiba hivyo kukiri wazi kuwa hakiheshimu utawala wa kikatiba.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa