Home » » Mamlaka ya Bunge la Katiba yana mipaka

Mamlaka ya Bunge la Katiba yana mipaka

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mipaka ambayo aliielezea Jaji Warioba ni kwa muktadha wa Tanzania, na siyo kwa jumla. Hoja yake ni kwamba kwa suala la Tanzania, Bunge la Mabadiliko ya Katiba linatanguliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ambayo ndiyo iliyokusanya maoni ya wananchi na kwa mantiki hiyo maoni hayo ndiyo yametengeneza Rasimu ya Katiba

Kumeibuka hoja inayolenga uwezo wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba kwa kuihusisha na Rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa kwenye bunge hilo na Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Baadhi wanajenga hoja kwamba mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba hayana mipaka, wakati wengine hoja yao inasema mamlaka ya bunge hilo ina mipaka.
Wale wanaosema mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba hayana mipaka, wanatengeneza hoja kwamba bunge hilo linaweza kuikataa Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa kwao, na kuwa na uwezo wa kutengeneza rasimu yao watakayoiwasilisha kwa wananchi kwa ajili ya kura ya maoni.
Hata hivyo, kwa wale wanaosema kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba mamlaka yake yana mipaka, wanajenga hoja kuwa bunge hilo halina mamlaka ya kuikataa rasimu ya msingi iliyowasilishwa kwao, na kwamba mamlaka ya bunge hilo ni kuiboresha rasimu hiyo, lakini siyo kuikataa kama ilivyo.
Wiki moja iliyopita, makala ya Profesa Issa Shivji, ilichapishwa kwenye gazeti la Raia Mwema la Machi 5- 11, 2014, ambapo alieleza msimamo wake kwamba mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba hayana mipaka.
Profesa Shivji alikuwa akijibu hoja ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, ambaye alieleza kuwa Mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba yana mipaka.
Mipaka ambayo aliielezea Jaji Warioba ni kwa muktadha wa Tanzania, na siyo kwa jumla. Hoja yake ni kwamba kwa suala la Tanzania, Bunge la Mabadiliko ya Katiba linatanguliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ambayo ndiyo iliyokusanya maoni ya wananchi na kwa mantiki hiyo maoni hayo ndiyo yametengeneza Rasimu ya Katiba.
Profesa Shivji alipinga wale wanaokuja na hoja kwamba Bunge la Mabadiliko ya Katiba lina mipaka, akisema hoja hiyo haiwakilishi dhana ya nguvu ya mpiga kura. Napinga kwa kusema kuwa ni Profesa Shivji ndiye hoja yake haiwakilishi dhana ya nguvu ya mpiga kura.
Nguvu ya mpiga kura
Nguvu ya mpiga kura ni mamlaka yenye nguvu kuunda au msingi wa mabadiliko ya katiba na kutengeneza msingi wenye thamani utakaoongoza Serikali ya taifa husika.
Nguvu hiyo haitoki ndani ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba. Inarithiwa kutoka kwa watu. Bunge la Mabadiliko ya Katiba linaweza kutumia mamlaka hayo kwa ajili au kwa niaba ya wananchi. Bunge la Mabadiliko ya Katiba linapata mamlaka hayo kutokana na ridhaa ya wananchi ambao ndiyo wanaoamua namna ya kutawaliwa.
Hiyo ndiyo sababu kwa nini nguvu ya mpiga kura ni mamlaka ya enzi. Ni mamlaka ya enzi kwa sababu imetokana na wananchi. Wamiliki sahihi wa mamlaka ya mpiga kura ni taifa, ambalo ndiyo lenye nguvu na haliwezi kuwa na mipaka ya muundo wowote wa sheria chanya. Bunge la Mabadiliko ya Katiba pia ni wawakilishi wa wananchi katika hamu yao ya kutafuta sheria mama.
Bunge la Mabadiliko ya Katiba lazima wakati wote linafanya kazi kwa jina na chini ya maagizo kutoka kwa wananchi, ambao kwa wakati wowote wanaweza kutengua maagizo yao kwa kupitia njia za kisiasa. Ni ridhaa ya wananchi ambao ndio wanaweza kulifanya Bunge la Mabadiliko ya Katiba kuwa na mamlaka.
Kama hiyo inakubalika ni wazi kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba halina mamlaka zaidi ya yale waliyoridhia wananchi wenyewe. Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni chombo cha uwakilishi tu, ni mtumishi wa wananchi. Mamlaka yake ni yale ya kuagizwa au kutumwa. Aliyeagizwa hawezi kuwa na mamlaka zaidi ya mtu aliyemtuma. Maneno ya Alexander Hamilton, aliyoyatoa kwenye gazeti la Federalist namba 78 “…hakuna nafasi inayotegemea kanuni zilizo sahihi zaidi ya kila kitendo cha mwenye mamlaka aliyeagiza, kifanyike kama utaratibu ulivyowekwa kinyume chake ni bure…Kukataa hili neno ni kuthibitisha kuwa naibu ni mkubwa kuliko mkuu wake, kwamba mtumishi yuko juu ya mwajiri wake, kwamba wawakilishi wa wananchi wako juu kuliko wananchi wenyewe, kwamba watu wanaotenda kwa mamlaka ya majukumu yao inawezekana ndivyo mamlaka yao yanavyoruhusu, lakini pia ndivyo wanavyokatazwa.”
Kwa madhumuni gani Bunge la Mabadiliko ya Katiba linajikuta limekuwepo? Bunge limeundwa kwa madhumuni pekee ya kutengeneza katiba.
Katiba ni shughuli ya taifa zima, siyo kikundi cha watu. Kama hilo linakubalika, ni wazi kuwa Bunge la Katiba ni wawakilishi wa taifa zima. Kwa madhumuni ya kiutendaji, wote tunakubali kuwa taifa lote haliwezi kukutana kwenye sehemu moja kutengeneza katiba. Ni wazi kuwa lazima kuwepo wawakilishi wa kuwakilisha taifa lote. Tangu kutangazwa kuwa Bunge la Katiba limeundwa kwa kuzingatia uwakilishi, jukumu la wawakilishi ndani ya Bunge ni kuendeleza maoni ya wale wanaowawakilisha. Hawawezi kudharau maoni ya wale wanaowawakilisha.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa suala la Tanzania ni chombo cha kukusanya maoni. Chombo hiki kimefanya kazi ya kukusanya maoni ya wananchi wa Tanzania. Maoni yanayowasilishwa na Tume hii ni maoni ya wananchi wa Tanzania. Wameweka hoja ambazo ni kwa vipi Wajumbe wa Bunge la Katiba wanaweza kuzishughulikia au kutozishughulikia.
Maoni hayo yanatengeneza mamlaka kwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba. Wajumbe wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba, kama watumishi wa wananchi wa Tanzania hawategemewi kuyashusha hadhi maoni hayo, kwa sababu kwa kufanya hivyo itakuwa wanafanya kitu ambacho hawana mamlaka nacho.
Wananchi wa Tanzania kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba wameeleza matakwa yao ya namna wanavyotaka kutawaliwa. Ridhaa hiyo imekwishaelezewa katika Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa kwenye Bunge.
Bunge linachotakiwa kufanya katika mazingira haya ni kuboresha maandiko, lakini siyo kuyadharau matakwa hayo. Kuleta vitu vipya, ambavyo wananchi hawakuvizungumzia, na kudharau maoni yao, ambayo waliyazungumza mbele ya Tume, itakuwa ni kitendo cha udhalimu na siyo demokrasia.
Kama hiyo inakubalika, ni wazi kuwa jukumu la Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni lile la mtumishi na siyo mwajiri. Wakati wananchi tayari wameeleza matamanio yao ya namna gani wanataka watawaliwe, Bunge la Mabadiliko ya Katiba haliwezi kujitangazia mamlaka ya enzi.
Jukumu lake kwa mantiki hiyo limewekewa mipaka na maoni ya wananchi wenyewe. Linachotakiwa kufanya ni kuboresha maoni hayo, lakini siyo kudharau yalikotoka. Mamlaka ya kutengeneza katiba imeasisiwa na wananchi na siyo Bunge la Mabadiliko ya Katiba, ambalo ni chombo cha uwakilishi wa wananchi.
Ninakubali kwa dhati kuwa mamlaka ya mpiga kura hayawezi kuwekewa mipaka na aina yoyote ya sheria chanya. Swali la msingi, nani anabeba mamlaka ya mpiga kura?
Anayebeba mamlaka ya mpiga kura ni mwananchi wa Tanzania, na siyo Bunge la Mabadiliko ya Katiba. Demokrasia inamtambua mwananchi kuwa ndiye mmiliki halali wa mamlaka ya mpiga kura. Kama hiyo inakubalika, kama msingi wa kanuni, ni wazi kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba la sasa lililopo Dodoma, hawana mamlaka ya kudharau yale ambayo wamiliki wa mamlaka ya kupiga kura wameyasema mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Kukataa hilo itakuwa ni kuthibitisha kuwa mtumishi ni mkubwa kuliko mwajiri wake. Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni chombo kinacho wakilisha wananchi. Kwa namna hiyo, chombo hicho hakina mamlaka ya kudharau kile ambacho wananchi (mwajiri) wameridhia. Ni muhimu kuelewa kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni watunga sheria wa kawaida, ni chombo cha ‘uwakilishi’, kilichoundwa kwa kuchaguliwa na wananchi.
Bunge la Mabadiliko ya Katiba siyo watu. Mbaya zaidi, hakuna mjumbe wa Bunge aliyechaguliwa na wananchi kwa madhumuni ya kazi ya kutunga Katiba. Hata wabunge wa Bunge la Jamhuri na Wawakilishi wa Zanzibar ambao ni sehemu ya waliounda Bunge hilo, hawakuchaguliwa kwa madhumuni ya kutunga katiba. Kazi yao ni kutunga sheria za kawaida tu.
Bwana Justice John Laws, alitufundisha kuwa kwa hoja ya msingi wa kanuni, kudumu na kustawi kwa demokrasia…kunahitaji wale wanaoitekeleza demokrasia, nguvu ya kisiasa lazima iweke mipaka ya wanachotaka kukifanya; kuweka mpaka kwa kile ambacho hawatakiwi kukivuka.
Kama hii ni sawa, kazi ya nguvu ya demokrasia siyo kuwa na amri zote peke yake. Wajumbe wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba wanatwaa madaraka ya kisiasa, ambacho siyo kuteka amri zote, kwa sababu wao ni wawakilishi. Kuendelea kama alivyoshauri Profesa Shivji. Profesa Shivji lazima atambue kuwa kila neno la kidhalimu ni ‘ neno langu la sheria’. Bunge la demokrasia lina mamlaka ya enzi nyuma ya pazia ni kama vile maneno matupu. Uteuzi wake hauwezi kuwa na kinga ya kutokuwa na jukumu la kidhalimu. Asante demokrasia hairuhusu hayo.
Profesa Shivji alimtaka Jaji Warioba kutaja chanzo cha msimamo wake kwamba mamlaka ya mpiga kura yana mipaka. Kwanza nimnusuru Jaji Warioba. Dhana maarufu ya mamlaka ya mpiga kura ilitolewa na Emmanuel Joseph Sieye (a.k.a Abbe ‘Sieye’s) na kufuatiwa na Carl Schmitt, William E. Scheuerman, Antonio Negri na Andreas Kalyvas(nina vyanzo vyake na ninaweza kutoa kwa yeyote anayetaka).
Katika kitabu chake cha kisiasa, ‘Ni upi muhimili wa tatu?’ kilichochapishwa mwaka 1789, Mfaransa huyo alifafanua kuwa taifa lina haki ya kumiliki mamlaka ya mpiga kura, kama vile kuwezesha kupitisha katiba ya Ufaransa. ‘Taifa,’ aliandika liko juu ya kila kitu. Ni chanzo cha kila kitu. Matakwa yake mara zote ni sheria; kimsingi ni sheria kamili. Ni zaidi ya taifa, siku zote kuna sheria za asili.”
Sieye’s alijenga hoja kuwa mamlaka ya mpiga kura kiasili yana mipaka. Kwake Sieye’s, mamlaka ya mpiga kura siyo mamlaka holela. Ni mamlaka, ambayo mara zote mipaka yake inatokana na umuhimu wa taifa.
Kulingana na William E. Scheuerman katika kitabu chake cha Mapinduzi na Katiba, kilichochapishwa na David Dyzenhaus, akisema Sheria kama Siasa: akielezea ukosoaji wa Carl Schmitt katika mambo ya misimamo kilichochapishwa mwaka 1998, “Ni pale tu bunge la wawakilishi litakapoheshimu matakwa ya wananchi, linaweza kujipambanua kwa kuwa na sababu na kutenda haki na kupiga kura kwa taifa lote bila kuongeza mambo.”
Sieye’s aliendelea kutetea kuwa, utendaji wa mamlaka ya mpiga kura ni moja ya mpaka wa msingi. “Ni lazima ifuate ridhaa ya wananchi.” Ni lazima itende kwa jina la wananchi. Mamlaka yake siyo ya kipekee, bali yanawekewa mipaka na matamanio ya waliotoa madaraka. Maana ya neno walilotoa, lina maana wananchi kwa ujumla wao kama taifa.
“Kuzungumzia mamlaka ya mpiga kura,” ameandika Antonio Negri katika kitabu chake cha Mamlaka ya Mpiga Kura na Taifa la sasa, kilichochapishwa mwaka 1999, “ni kuzungumzia demokrasia. Katika miaka ya sasa dhana mbili mara zote zimekuwa zikishabihiana.” “Demokrasia kwa asili yake imerithi mipaka.
Mmojawapo wanaoshikilia madaraka kwa niaba ya wengine, hawawezi na hawatakiwi kuvuka mamlaka waliyopewa. Waliopewa mamlaka hawatakiwi kutenda kwa matakwa yao, bali kwa masilahi ya wale waliompa mamlaka. Tangu mamlaka ya mpiga kura yalipochukua sehemu ya demokrasia, ni muhimu kuwa mchakato wa kutunga Katiba kupitia Bunge la Kutunga Katiba iwe ya ushirikishwaji.
Mamlaka ya mpiga kura, kwa namna nyingine siyo kama ajali kuwa msingi wa kutunga katiba. Ni mamlaka ya kutunga katiba kwa pamoja. Kama alivyoelezea Andreas Kalyvas katika kitabu chake cha msingi wa kanuni na demokrasia na nadharia za kisiasa, kilichochapishwa mwaka 2006 kwenye jarida la Philosophy and Social Criticism , “neno mpiga kura” lina maana kutengeneza, kuunda au kitendo cha kutengeneza kwa pamoja au kutengeneza katiba kwa pamoja.
Demokrasia, kama mamlaka ya mpiga kura, inahitaji ushirikishwaji wa wananchi katika kupitisha sheria zote, ikiwemo sheria za msingi. Inahusisha uthibitisho wa mgawanyo sawa wa shughuli na mamlaka ya wananchi wote.” Inahitaji ushirikishwaji wa wananchi wote katika kutunga sheria, hata kama kwa sababu za msingi kuwa hawawezi kushiriki moja kwa moja.
Hata hivyo, kama kuna fursa pekee ya wananchi ni kushiriki moja kwa moja katika maamuzi ya kisiasa utakuwepo, kwa tukio kama la mabadiliko ya katiba, demokrasia inahitaji uwepo wa ushirikishwaji wa wananchi kwa kiwango cha juu, moja ya jambo la msingi la dhana ya demokrasia ni kuwa na uhalisia. Kiukweli ni ngumu kumuhusisha kila mtu, unapotaka kutekeleza demokrasia halisi, hata kama ni suala la kanuni, ni afahdali wananchi wakawekwa pembeni wakati wa mchakato wa kutunga katiba, hatakiwi kuruhusiwa kuwa waandishi wa katiba ambayo inawahusu. Hivyo ndivyo Profesa Shivji ambaye anaamini Bunge la Mabadiliko ya Katiba linaweza kudharau yale wananchi wa Tanzania waliyosema mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Profesa Shivji anajenga hoja kuwa maoni yaliyowasilishwa kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba hayana msingi kwa sababu idadi ya waliotoa maoni ni ndogo mno. Na kwamba yanafaa kuachwa. Fikira hizo hazikubariki kwakuwa ilikuwa ni fursa kwa yeyote aliyealikwa kutoa maoni yake. Hakukuwa na ushurutishwaji, wala vitisho. Kama mtu hakutokea kuwasilisha maoni yake, amepoteza fursa yake. Hawawezi sasa kusikilizwa malalamiko yao. Nashangazwa na Profesa Shivji aliyetoa hoja hiyo.
Ni tafasiri isiyo rasmi kutoka kwenye mhadhara wa Beatus Malima, mhadhiri msaidizi katika Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Anapatikana kwa baruapepe: malima@mawalla.co.tz au namba ya simu +255 784 313139.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa