Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Kumeibuka hoja inayolenga uwezo wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba
kwa kuihusisha na Rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa kwenye bunge
hilo na Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Baadhi wanajenga hoja kwamba
mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba hayana mipaka, wakati wengine
hoja yao inasema mamlaka ya bunge hilo ina mipaka.
Wale wanaosema mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya
Katiba hayana mipaka, wanatengeneza hoja kwamba bunge hilo linaweza
kuikataa Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa kwao, na kuwa na uwezo wa
kutengeneza rasimu yao watakayoiwasilisha kwa wananchi kwa ajili ya kura
ya maoni.
Hata hivyo, kwa wale wanaosema kuwa Bunge la
Mabadiliko ya Katiba mamlaka yake yana mipaka, wanajenga hoja kuwa bunge
hilo halina mamlaka ya kuikataa rasimu ya msingi iliyowasilishwa kwao,
na kwamba mamlaka ya bunge hilo ni kuiboresha rasimu hiyo, lakini siyo
kuikataa kama ilivyo.
Wiki moja iliyopita, makala ya Profesa Issa
Shivji, ilichapishwa kwenye gazeti la Raia Mwema la Machi 5- 11, 2014,
ambapo alieleza msimamo wake kwamba mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya
Katiba hayana mipaka.
Profesa Shivji alikuwa akijibu hoja ya Mwenyekiti
wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, ambaye alieleza
kuwa Mamlaka ya Bunge la Mabadiliko ya Katiba yana mipaka.
Mipaka ambayo aliielezea Jaji Warioba ni kwa
muktadha wa Tanzania, na siyo kwa jumla. Hoja yake ni kwamba kwa suala
la Tanzania, Bunge la Mabadiliko ya Katiba linatanguliwa na Tume ya
Mabadiliko ya Katiba, ambayo ndiyo iliyokusanya maoni ya wananchi na kwa
mantiki hiyo maoni hayo ndiyo yametengeneza Rasimu ya Katiba.
Profesa Shivji alipinga wale wanaokuja na hoja
kwamba Bunge la Mabadiliko ya Katiba lina mipaka, akisema hoja hiyo
haiwakilishi dhana ya nguvu ya mpiga kura. Napinga kwa kusema kuwa ni
Profesa Shivji ndiye hoja yake haiwakilishi dhana ya nguvu ya mpiga
kura.
Nguvu ya mpiga kura
Nguvu ya mpiga kura ni mamlaka yenye nguvu kuunda
au msingi wa mabadiliko ya katiba na kutengeneza msingi wenye thamani
utakaoongoza Serikali ya taifa husika.
Nguvu hiyo haitoki ndani ya Bunge la Mabadiliko ya
Katiba. Inarithiwa kutoka kwa watu. Bunge la Mabadiliko ya Katiba
linaweza kutumia mamlaka hayo kwa ajili au kwa niaba ya wananchi. Bunge
la Mabadiliko ya Katiba linapata mamlaka hayo kutokana na ridhaa ya
wananchi ambao ndiyo wanaoamua namna ya kutawaliwa.
Hiyo ndiyo sababu kwa nini nguvu ya mpiga kura ni
mamlaka ya enzi. Ni mamlaka ya enzi kwa sababu imetokana na wananchi.
Wamiliki sahihi wa mamlaka ya mpiga kura ni taifa, ambalo ndiyo lenye
nguvu na haliwezi kuwa na mipaka ya muundo wowote wa sheria chanya.
Bunge la Mabadiliko ya Katiba pia ni wawakilishi wa wananchi katika hamu
yao ya kutafuta sheria mama.
Bunge la Mabadiliko ya Katiba lazima wakati wote
linafanya kazi kwa jina na chini ya maagizo kutoka kwa wananchi, ambao
kwa wakati wowote wanaweza kutengua maagizo yao kwa kupitia njia za
kisiasa. Ni ridhaa ya wananchi ambao ndio wanaweza kulifanya Bunge la
Mabadiliko ya Katiba kuwa na mamlaka.
Kama hiyo inakubalika ni wazi kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba
halina mamlaka zaidi ya yale waliyoridhia wananchi wenyewe. Bunge la
Mabadiliko ya Katiba ni chombo cha uwakilishi tu, ni mtumishi wa
wananchi. Mamlaka yake ni yale ya kuagizwa au kutumwa. Aliyeagizwa
hawezi kuwa na mamlaka zaidi ya mtu aliyemtuma. Maneno ya Alexander
Hamilton, aliyoyatoa kwenye gazeti la Federalist namba 78 “…hakuna
nafasi inayotegemea kanuni zilizo sahihi zaidi ya kila kitendo cha
mwenye mamlaka aliyeagiza, kifanyike kama utaratibu ulivyowekwa kinyume
chake ni bure…Kukataa hili neno ni kuthibitisha kuwa naibu ni mkubwa
kuliko mkuu wake, kwamba mtumishi yuko juu ya mwajiri wake, kwamba
wawakilishi wa wananchi wako juu kuliko wananchi wenyewe, kwamba watu
wanaotenda kwa mamlaka ya majukumu yao inawezekana ndivyo mamlaka yao
yanavyoruhusu, lakini pia ndivyo wanavyokatazwa.”
Kwa madhumuni gani Bunge la Mabadiliko ya Katiba
linajikuta limekuwepo? Bunge limeundwa kwa madhumuni pekee ya
kutengeneza katiba.
Katiba ni shughuli ya taifa zima, siyo kikundi cha
watu. Kama hilo linakubalika, ni wazi kuwa Bunge la Katiba ni
wawakilishi wa taifa zima. Kwa madhumuni ya kiutendaji, wote tunakubali
kuwa taifa lote haliwezi kukutana kwenye sehemu moja kutengeneza katiba.
Ni wazi kuwa lazima kuwepo wawakilishi wa kuwakilisha taifa lote. Tangu
kutangazwa kuwa Bunge la Katiba limeundwa kwa kuzingatia uwakilishi,
jukumu la wawakilishi ndani ya Bunge ni kuendeleza maoni ya wale
wanaowawakilisha. Hawawezi kudharau maoni ya wale wanaowawakilisha.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa suala la Tanzania
ni chombo cha kukusanya maoni. Chombo hiki kimefanya kazi ya kukusanya
maoni ya wananchi wa Tanzania. Maoni yanayowasilishwa na Tume hii ni
maoni ya wananchi wa Tanzania. Wameweka hoja ambazo ni kwa vipi Wajumbe
wa Bunge la Katiba wanaweza kuzishughulikia au kutozishughulikia.
Maoni hayo yanatengeneza mamlaka kwa Bunge la
Mabadiliko ya Katiba. Wajumbe wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba, kama
watumishi wa wananchi wa Tanzania hawategemewi kuyashusha hadhi maoni
hayo, kwa sababu kwa kufanya hivyo itakuwa wanafanya kitu ambacho hawana
mamlaka nacho.
Wananchi wa Tanzania kupitia Tume ya Mabadiliko ya
Katiba wameeleza matakwa yao ya namna wanavyotaka kutawaliwa. Ridhaa
hiyo imekwishaelezewa katika Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa kwenye
Bunge.
Bunge linachotakiwa kufanya katika mazingira haya
ni kuboresha maandiko, lakini siyo kuyadharau matakwa hayo. Kuleta vitu
vipya, ambavyo wananchi hawakuvizungumzia, na kudharau maoni yao, ambayo
waliyazungumza mbele ya Tume, itakuwa ni kitendo cha udhalimu na siyo
demokrasia.
Kama hiyo inakubalika, ni wazi kuwa jukumu la
Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni lile la mtumishi na siyo mwajiri.
Wakati wananchi tayari wameeleza matamanio yao ya namna gani wanataka
watawaliwe, Bunge la Mabadiliko ya Katiba haliwezi kujitangazia mamlaka
ya enzi.
Jukumu lake kwa mantiki hiyo limewekewa mipaka na
maoni ya wananchi wenyewe. Linachotakiwa kufanya ni kuboresha maoni
hayo, lakini siyo kudharau yalikotoka. Mamlaka ya kutengeneza katiba
imeasisiwa na wananchi na siyo Bunge la Mabadiliko ya Katiba, ambalo ni
chombo cha uwakilishi wa wananchi.
Ninakubali kwa dhati kuwa mamlaka ya mpiga kura
hayawezi kuwekewa mipaka na aina yoyote ya sheria chanya. Swali la
msingi, nani anabeba mamlaka ya mpiga kura?
Anayebeba mamlaka ya mpiga kura ni mwananchi wa
Tanzania, na siyo Bunge la Mabadiliko ya Katiba. Demokrasia inamtambua
mwananchi kuwa ndiye mmiliki halali wa mamlaka ya mpiga kura. Kama hiyo
inakubalika, kama msingi wa kanuni, ni wazi kuwa Bunge la Mabadiliko ya
Katiba la sasa lililopo Dodoma, hawana mamlaka ya kudharau yale ambayo
wamiliki wa mamlaka ya kupiga kura wameyasema mbele ya Tume ya
Mabadiliko ya Katiba. Kukataa hilo itakuwa ni kuthibitisha kuwa mtumishi
ni mkubwa kuliko mwajiri wake. Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni chombo
kinacho wakilisha wananchi. Kwa namna hiyo, chombo hicho hakina mamlaka
ya kudharau kile ambacho wananchi (mwajiri) wameridhia. Ni muhimu
kuelewa kuwa Bunge la Mabadiliko ya Katiba ni watunga sheria wa kawaida,
ni chombo cha ‘uwakilishi’, kilichoundwa kwa kuchaguliwa na wananchi.
Bunge la Mabadiliko ya Katiba siyo watu. Mbaya
zaidi, hakuna mjumbe wa Bunge aliyechaguliwa na wananchi kwa madhumuni
ya kazi ya kutunga Katiba. Hata wabunge wa Bunge la Jamhuri na
Wawakilishi wa Zanzibar ambao ni sehemu ya waliounda Bunge hilo,
hawakuchaguliwa kwa madhumuni ya kutunga katiba. Kazi yao ni kutunga
sheria za kawaida tu.
Bwana Justice John Laws, alitufundisha kuwa kwa hoja ya msingi
wa kanuni, kudumu na kustawi kwa demokrasia…kunahitaji wale
wanaoitekeleza demokrasia, nguvu ya kisiasa lazima iweke mipaka ya
wanachotaka kukifanya; kuweka mpaka kwa kile ambacho hawatakiwi
kukivuka.
Kama hii ni sawa, kazi ya nguvu ya demokrasia siyo
kuwa na amri zote peke yake. Wajumbe wa Bunge la Mabadiliko ya Katiba
wanatwaa madaraka ya kisiasa, ambacho siyo kuteka amri zote, kwa sababu
wao ni wawakilishi. Kuendelea kama alivyoshauri Profesa Shivji. Profesa
Shivji lazima atambue kuwa kila neno la kidhalimu ni ‘ neno langu la
sheria’. Bunge la demokrasia lina mamlaka ya enzi nyuma ya pazia ni kama
vile maneno matupu. Uteuzi wake hauwezi kuwa na kinga ya kutokuwa na
jukumu la kidhalimu. Asante demokrasia hairuhusu hayo.
Profesa Shivji alimtaka Jaji Warioba kutaja chanzo
cha msimamo wake kwamba mamlaka ya mpiga kura yana mipaka. Kwanza
nimnusuru Jaji Warioba. Dhana maarufu ya mamlaka ya mpiga kura ilitolewa
na Emmanuel Joseph Sieye (a.k.a Abbe ‘Sieye’s) na kufuatiwa na Carl
Schmitt, William E. Scheuerman, Antonio Negri na Andreas Kalyvas(nina
vyanzo vyake na ninaweza kutoa kwa yeyote anayetaka).
Katika kitabu chake cha kisiasa, ‘Ni upi muhimili
wa tatu?’ kilichochapishwa mwaka 1789, Mfaransa huyo alifafanua kuwa
taifa lina haki ya kumiliki mamlaka ya mpiga kura, kama vile kuwezesha
kupitisha katiba ya Ufaransa. ‘Taifa,’ aliandika liko juu ya kila kitu.
Ni chanzo cha kila kitu. Matakwa yake mara zote ni sheria; kimsingi ni
sheria kamili. Ni zaidi ya taifa, siku zote kuna sheria za asili.”
Sieye’s alijenga hoja kuwa mamlaka ya mpiga kura
kiasili yana mipaka. Kwake Sieye’s, mamlaka ya mpiga kura siyo mamlaka
holela. Ni mamlaka, ambayo mara zote mipaka yake inatokana na umuhimu wa
taifa.
Kulingana na William E. Scheuerman katika kitabu
chake cha Mapinduzi na Katiba, kilichochapishwa na David Dyzenhaus,
akisema Sheria kama Siasa: akielezea ukosoaji wa Carl Schmitt katika
mambo ya misimamo kilichochapishwa mwaka 1998, “Ni pale tu bunge la
wawakilishi litakapoheshimu matakwa ya wananchi, linaweza kujipambanua
kwa kuwa na sababu na kutenda haki na kupiga kura kwa taifa lote bila
kuongeza mambo.”
Sieye’s aliendelea kutetea kuwa, utendaji wa
mamlaka ya mpiga kura ni moja ya mpaka wa msingi. “Ni lazima ifuate
ridhaa ya wananchi.” Ni lazima itende kwa jina la wananchi. Mamlaka yake
siyo ya kipekee, bali yanawekewa mipaka na matamanio ya waliotoa
madaraka. Maana ya neno walilotoa, lina maana wananchi kwa ujumla wao
kama taifa.
“Kuzungumzia mamlaka ya mpiga kura,” ameandika
Antonio Negri katika kitabu chake cha Mamlaka ya Mpiga Kura na Taifa la
sasa, kilichochapishwa mwaka 1999, “ni kuzungumzia demokrasia. Katika
miaka ya sasa dhana mbili mara zote zimekuwa zikishabihiana.”
“Demokrasia kwa asili yake imerithi mipaka.
Mmojawapo wanaoshikilia madaraka kwa niaba ya
wengine, hawawezi na hawatakiwi kuvuka mamlaka waliyopewa. Waliopewa
mamlaka hawatakiwi kutenda kwa matakwa yao, bali kwa masilahi ya wale
waliompa mamlaka. Tangu mamlaka ya mpiga kura yalipochukua sehemu ya
demokrasia, ni muhimu kuwa mchakato wa kutunga Katiba kupitia Bunge la
Kutunga Katiba iwe ya ushirikishwaji.
Mamlaka ya mpiga kura, kwa namna nyingine siyo
kama ajali kuwa msingi wa kutunga katiba. Ni mamlaka ya kutunga katiba
kwa pamoja. Kama alivyoelezea Andreas Kalyvas katika kitabu chake cha
msingi wa kanuni na demokrasia na nadharia za kisiasa, kilichochapishwa
mwaka 2006 kwenye jarida la Philosophy and Social Criticism , “neno
mpiga kura” lina maana kutengeneza, kuunda au kitendo cha kutengeneza
kwa pamoja au kutengeneza katiba kwa pamoja.
Demokrasia, kama mamlaka ya mpiga kura, inahitaji
ushirikishwaji wa wananchi katika kupitisha sheria zote, ikiwemo sheria
za msingi. Inahusisha uthibitisho wa mgawanyo sawa wa shughuli na
mamlaka ya wananchi wote.” Inahitaji ushirikishwaji wa wananchi wote
katika kutunga sheria, hata kama kwa sababu za msingi kuwa hawawezi
kushiriki moja kwa moja.
Hata hivyo, kama kuna fursa pekee ya wananchi ni
kushiriki moja kwa moja katika maamuzi ya kisiasa utakuwepo, kwa tukio
kama la mabadiliko ya katiba, demokrasia inahitaji uwepo wa
ushirikishwaji wa wananchi kwa kiwango cha juu, moja ya jambo la msingi
la dhana ya demokrasia ni kuwa na uhalisia. Kiukweli ni ngumu
kumuhusisha kila mtu, unapotaka kutekeleza demokrasia halisi, hata kama
ni suala la kanuni, ni afahdali wananchi wakawekwa pembeni wakati wa
mchakato wa kutunga katiba, hatakiwi kuruhusiwa kuwa waandishi wa katiba
ambayo inawahusu. Hivyo ndivyo Profesa Shivji ambaye anaamini Bunge la
Mabadiliko ya Katiba linaweza kudharau yale wananchi wa Tanzania
waliyosema mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Profesa Shivji anajenga hoja kuwa maoni yaliyowasilishwa kwenye
Tume ya Mabadiliko ya Katiba hayana msingi kwa sababu idadi ya waliotoa
maoni ni ndogo mno. Na kwamba yanafaa kuachwa. Fikira hizo hazikubariki
kwakuwa ilikuwa ni fursa kwa yeyote aliyealikwa kutoa maoni yake.
Hakukuwa na ushurutishwaji, wala vitisho. Kama mtu hakutokea kuwasilisha
maoni yake, amepoteza fursa yake. Hawawezi sasa kusikilizwa malalamiko
yao. Nashangazwa na Profesa Shivji aliyetoa hoja hiyo.
Ni tafasiri isiyo rasmi kutoka kwenye mhadhara wa
Beatus Malima, mhadhiri msaidizi katika Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam. Anapatikana kwa baruapepe: malima@mawalla.co.tz au
namba ya simu +255 784 313139.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment