Home » » Sitta aeleza mizengwe ya uchaguzi

Sitta aeleza mizengwe ya uchaguzi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Aliyewahi kuwa Spika wa Bunge la Tisa, Samuel Sitta ameelezea changamoto alizopata katika mchakato wa uchaguzi uliomweka madarakani kuwa Mwenyekiti wa Bunge la Katiba baada ya kupata kura 487. Katika uchaguzi huo, Sitta alimshinda mpinzani wake Hashim Rungwe kwa tofauti ya kura 418. Awali Sitta alipata upinzani wa ndani ya chama kutoka kwa aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge ambaye alitajwa kutaka kuwania nafasi hiyo.
Upinzani huo uliibua mvutano mkali na kusababisha makundi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo yalizimwa na  uongozi wa chama hicho kuwaita Sitta na Chenge na kuwataka wakubaliane nani kati yao, asimame kugombea nafasi hiyo.
Sitta azushiwa ugonjwa
Baada ya Chenge kumpisha mwenzake Sitta awanie nafasi hiyo na Samia Suluhu Hassan kuwa makamu wake, kulisambazwa taarifa katika mitandao ya kijamii kuwa Sitta ni mgonjwa mahtuti na amepelekwa hospitali kwa matibabu.
Taarifa hizo zilianza kusambaa Machi 12 kuanzia saa nne usiku, hali ambayo iliibua sintofahamu kwa baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo wanaomuunga mkono mgombea huyo.
Baada ya kurudisha fomu za kugombea nafasi hiyo, Sitta alizungumzia uvumi huo na kusema, “Wabaya wangu ndio waliosambaza hizo taarifa. Mimi ni mzima na nimetoka kurudisha fomu za kugombea Uwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba.”
Anaongeza, “Mimi ni kiongozi ninayetenda haki kwa kila mtu jambo ambalo linawaudhi watu wanaotaka kupendelewa kila jambo. Sikushangazwa na taarifa hizo kwa sababu nilipoteuliwa na CCM kugombea nafasi hii wapo waliopinga na kusema kuwa siwezi kugombea kwa sababu mimi ni waziri.”
Sitta anasema kuwa licha ya kupitishwa na chama chake kugombea nafasi hiyo, alishangazwa na kitendo cha aliyewahi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk. Terezya Huvisa kuchukua fomu za kugombea nafasi hiyo.
“Huvisa ana nguvu fulani nyuma yake. Asingeweza kuibuka tu na kukiuka uamuzi wa chama na kuchukua fomu za kugombea maana kamati iliyonipitisha ilikuwa chini ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,” alisema.
Chanzo;Mwananchi 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa