Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mbunge wa Kinondoni, Mussa Azan Zungu
Akichangia mjadala wa Bajeti ya Serikali jana bungeni mjini Dodoma, Mbunge wa Kinondoni, Mussa Azan Zungu (pichani) alisema kuwa makampuni ya kigeni yanayowekeza kwenye sekta ya gesi yana tabia ya kufanya udangayifu ili kukwepa kodi na kuikosesha Serikali mapato inayostahili.
“Makampuni haya yamezoea kufanya udanganyifu juu ya shughuli zake na kiasi halisi cha uzalishaji wao, ni lazima uwekwe utaratibu mzuri wa kuyafanya yalete taarifa zake sahihi serikalini ili kuepusha udanganyifu utakaoisababisha Serikali kukosa mapato inayostahili,” alisema Zungu.
Alisema kuwa kwa kutambua udanganyifu unaofanywa na makampuni hayo, tayari Serikali ya Marekani imetunga sheria inayoyataka makampuni ya nchi hiyo ambayo yanafanya kazi ya kuchimba mafuta na gesi katika nchi nyingine kupeleka taarifa sahihi za shughuli zake kwenye serikali yao.
Zungu alisema kuwa kutokana na umuhimu wa suala hilo, nchi nyingine za Magharibi pia zimeichukua sheria hiyo na kuitumia kuyabana makampuni ya uchimbaji wa mafuta na gesi ili kupata taarifa zao sahihi kwa lengo hilo hilo la kudhibiti udanganyifu unaofanywa na kampuni hizo.
Alisema Serikali ya Tanzania pia inaweza kutumia sheria hiyo kupata taarifa sahihi za kampuni hizo na kuzitumia kudhibiti mapato yake na kuziba mianya ya kampuni hizo kukwepa kulipa kodi halali serikalini.
“Serikali inaweza kuandaa utaratibu mzuri wa kuzilazimisha kampuni hizi kuzipatia nakala za taarifa hizo wanazopeleka kwenye Serikali yao, taarifa ambazo zitasaidia sana kuziba mianya ya ukwepaji kodi ambao hufanywa na kampuni hizo za kigeni,” alisema Zungu.
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment